28/02/2024
UPIGAJI SERENGETI WAMSH*TUA WAZIRI MKUU ACHUKUA HATUA KALI
Serengeti Media Centre
Waziri Kassim Majaliwa amemwagiza Kamanda wa Polisi mkoa wa Mara, ACP Salum Morcase kumk**ata Mkuu wa Kitengo cha Fedha na Uhasibu wa Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti,
Saad Mutunzi Ishabailu kwa kosa la kuhamisha sh. 213,748,085 kwa awamu nne kwa njia ya uhamisho wa ndani kwa kushirikiana na watumishi wa TAMISEMI na kuzitumia kwa matumizi yao binafsi.
Ametoa agizo hilo jana wakati akizungumza na madiwani na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti kwenye kikao kilichofanyika katika kwenye Halmashauri hiyo, mkoani Mara.
Waziri Mkuu amefikia hatua hiyo baada ya kuwaeleza watumishi na madiwani mbinu wanazotumia watumishi wachache wa baadhi ya Halmashauri ambao walikuwa wanashirikiana na watumishi watatu wa kitengo cha Treasury Single Account (TSA) kuiba fedha za umma.
Akitolea mfano juu ya mbinu zinazotumika na wachache hao, Waziri Mkuu aliwaeleza watumishi wa Halmashauri hiyo pamoja na Madiwani kwamba Juni 10, 2023 walitumia mwanya wa kuombea kibali fedha za bakaa kwa barua iliyosainiwa na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji Chatta Luleka.
Amesema Juni 21, mwaka jana Bw. Ishabailu alianza kufanya matumizi ya hizo fedha kwa kushirikiana na mfanyabiashara wa hapa Mugumu, Bw. Daudi Matinde Chacha kupitia kwenye akaunti zake za NMB na CRDB kwa kupitia miamala minne ya sh. milioni 76.3, sh. milioni 57.7, sh. milioni 47 na sh.milioni 32.5.
Amesema alipoulizwa na timu ya uchunguzi Matinde alikiri kuwa haidai fedha yoyote Halmashauri ya Serengeti isipokuwa mweka hazina huyo aliomba apitishie fedha zake kwenye akaunti zake kwa sababu zinahitajika haraka kwa matumizi ya ofisi. “Aliambiwa atoe shilingi milioni 189 akamkabidhi zote Ishabailu na zilizobakia (sh. milioni 24) akaambiwa abaki nazo,” amesema Waziri Mkuu.
Aliwasisitiza madiwani na watumishi kuwa makini na matumizi ya fedha za umma kwani serikali inapotafuta fedha na kuzileta kwenye Halmashauri zinatakuwa kutatua kero za wananchi walio wengi.